Romans 11

Mabaki Ya Israeli

1 aBasi nauliza: Je, Mungu amewakataa watu wake? La, hasha! Mimi mwenyewe ni Mwisraeli, tena uzao wa Ibrahimu kutoka kabila la Benyamini. 2 bMungu hajawakataa watu wake, ambao yeye aliwajua tangu mwanzo. Je, hamjui yale Maandiko yasemayo kuhusu Ilya, jinsi alivyomlalamikia Mungu kuhusu Israeli? 3 cAlisema, “Bwana, wamewaua manabii wako na kuzibomoa madhabahu zako, nimebaki mimi peke yangu, nao wanataka kuniua?” 4 dJe, Mungu alimjibuje? “Nimejibakizia watu elfu saba ambao hawajapiga magoti kumwabudu Baali.” 5 eVivyo hivyo pia, sasa wapo mabaki waliochaguliwa kwa neema ya Mungu. 6 fLakini ikiwa wamechaguliwa kwa neema, si tena kwa msingi wa matendo. Kama ingekuwa kwa matendo, neema isingekuwa neema tena.

7 gTuseme nini basi? Kile kitu ambacho Israeli alikitafuta kwa bidii hakukipata. Lakini waliochaguliwa walikipata. Waliobaki walifanywa wagumu, 8 hkama ilivyoandikwa: “Mungu aliwapa bumbuazi la mioyo,
macho ili wasiweze kuona,
na masikio ili wasiweze kusikia,
hadi leo.”

9 iNaye Daudi anasema: “Karamu zao na ziwe tanzi na mtego wa kuwanasa,
kitu cha kuwakwaza waanguke, na adhabu kwao.

10 jMacho yao yatiwe giza ili wasiweze kuona,
nayo migongo yao iinamishwe daima.”

Matawi Yaliyopandikizwa

11 kHivyo nauliza tena: Je, Waisraeli walijikwaa ili waanguke na kuangamia kabisa? La, hasha! Lakini kwa sababu ya makosa yao, wokovu umewafikia watu wa Mataifa, ili kuwafanya Waisraeli waone wivu. 12 lBasi ikiwa kukosa kwao kumekuwa utajiri mkubwa kwa ulimwengu, tena kama kuangamia kwao kumeleta utajiri kwa watu wa Mataifa, kurudishwa kwao kutaleta utajiri mkuu zaidi.

13 mSasa ninasema nanyi watu wa Mataifa. Maadamu mimi ni mtume kwa watu wa Mataifa, naitukuza huduma yangu 14 nili kuwafanya watu wangu waone wivu na hivyo kuwaokoa baadhi yao. 15 oKwa kuwa ikiwa kukataliwa kwao ni kupatanishwa kwa ulimwengu, kukubaliwa kwao si kutakuwa ni uhai baada ya kufa? 16 pKama sehemu ya donge la unga uliotolewa kuwa limbuko ni mtakatifu, basi unga wote ni mtakatifu, nalo shina kama ni takatifu, vivyo hivyo na matawi nayo.

17 qLakini kama baadhi ya matawi yalikatwa, nawe chipukizi la mzeituni mwitu ukapandikizwa mahali pao ili kushiriki unono pamoja na matawi mengine kutoka shina la mzeituni, 18 rbasi usijivune juu ya hayo matawi. Kama ukijivuna, kumbuka jambo hili: si wewe unayelishikilia shina, bali ni shina linalokushikilia wewe. 19Basi utasema, “Matawi yale yalikatwa ili nipate kupandikizwa katika hilo shina.” 20 sHii ni kweli. Matawi hayo yalikatwa kwa sababu ya kutokuamini kwake, lakini wewe umesimama tu kwa sababu ya imani. Kwa hiyo usijivune, bali simama kwa kuogopa. 21Kwa maana kama Mungu hakuyahurumia matawi ya asili, wala hatakuhurumia wewe.

22 tAngalia basi wema na ukali wa Mungu: Kwa wale walioanguka, ukali, bali kwako wewe wema wa Mungu, kama utadumu katika wema wake. La sivyo, nawe utakatiliwa mbali. 23 uWao nao wasipodumu katika kutokuamini kwao, watapandikizwa tena kwenye shina, kwa maana Mungu anao uwezo wa kuwapandikiza tena kwenye hilo shina. 24 vIkiwa wewe ulikatwa kutoka kile ambacho kwa asili ni mzeituni mwitu na kupandikizwa kinyume cha asili kwenye mzeituni uliopandwa, si rahisi zaidi matawi haya ya asili kupandikizwa tena kwenye shina lake la mzeituni!

Israeli Wote Wataokolewa

25 wNdugu zangu, ili msije mkajidai kuwa wenye hekima kuliko mlivyo, nataka mfahamu siri hii: Ugumu umewapata Israeli kwa sehemu hadi idadi ya watu wa Mataifa watakaoingia itimie. 26 xHivyo Israeli wote wataokolewa. Kama ilivyoandikwa: “Mkombozi atakuja kutoka Sayuni;
ataondoa kutokumcha Mungu katika Yakobo.

27 yHili ndilo agano langu nao
nitakapoziondoa dhambi zao.”

28 zKwa habari ya Injili, wao ni adui wa Mungu kwa ajili yenu, lakini kuhusu kule kuteuliwa kwao ni wapendwa, kwa ajili ya mababa zao wa zamani, 29 aakwa maana akishawapa watu karama, Mungu haziondoi, wala wito wake. 30 abKama vile ninyi wakati fulani mlivyokuwa waasi kwa Mungu lakini sasa mmepata rehema kwa sababu ya kutokutii kwao, 31hivyo nao Waisraeli wamekuwa waasi ili kwamba wao nao sasa waweze kupata rehema kwa ajili ya rehema za Mungu kwenu. 32 acKwa maana Mungu amewafunga wanadamu wote kwenye kuasi ili apate kuwarehemu wote.

Wimbo Wa Shukrani


33 adTazama jinsi kilivyo kina cha utajiri
wa hekima na maarifa ya Mungu!
Tazama jinsi ambavyo hukumu zake hazichunguziki,
na ambavyo njia zake zisivyotafutikana!

34 ae“Ni nani aliyeyafahamu mawazo ya Bwana?
Au ni nani ambaye amekuwa mshauri wake?”

35 af“Au ni nani aliyempa chochote
ili arudishiwe?”

36 agKwa maana vitu vyote vyatoka kwake, viko kwake na kwa ajili yake.
Utukufu ni wake milele! Amen.
Copyright information for SwhKC